Mwenyekiti wa Bodi GST Azindua Magari Mapya
GST yaaswa kuyatunza
📍Dodoma.
Watumishi wa Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania GST wametakiwa kuendelea kufanya kazi kwa bidii huku wakitumia vyema vitendea kazi kwa lengo la kutoa huduma bora za utafiti wa madini pamoja na huduma za maabara kwa wadau na wachimbaji wa Madini Hapa nchini.
Rai hiyo imetolewa Leo Februari 4, 2026 Jijini Dodoma na Mwenyekiti wa Bodi ya GST Bi. Yokbeth Myumbilwa wakati akizindua magari Mapya ya Taasisi hiyo kwa Niaba ya Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde ambapo amesisitiza watumishi kuendelea kufanya kazi kwa bidii.
Aidha, Bi. Myumbilwa amesema upatikanaji wa magari hayo utaboresha utendaji kazi wa taasisi hiyo kwa kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi.
Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa GST Mhandisi Ally Samaje ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuiwezesha GST na kuipatia magari hayo na kusema kuwa yataongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya Taasisi.
Pia, Mhandisi Samaje ameeleza kuwa upatikanaji wa magari hayo utaongeza kasi katika kutekeleza majukumu yake ikiwemo la kufanya utafiti wa madini kwenye maeneo mbalimbali ya nchi yetu.
Aidha, Mha. Samaje ameahidi kuendelea kusimamia na kutunza mali za taasisi ikiwemo magari hayo ili yaweze kutumika vyema katika kutekeleza majukumu ya taasisi ikiwemo kufanya shughuli za ugani.

